Jumanne , 20th Aug , 2019

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi, Mkoa wa Dar es salaam, Musa Kilakala, amependekeza kupimwa kwa baadhi ya Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kile alichodai kuna baadhi yao

wanajihusisha na matendo yasiyokuwa na maadili ikiwemo kujihusisha na mapenzi ya jinsia moja.

Musa Kilakala ametoa kauli hiyo wakati wa uzinduzi wa Kampeni ya Tanga Kijani, iliyofanyika mkoani Tanga, ambapo amemuomba Spika Ndugai kama ambavyo Bunge limeazimia kupimwa ulevi kwa Wabunge, pia liwapime Wabunge ambao wanahisiwa wanajihusisha na vitendo hivyo.

"Kuna mkakati mkubwa kuna baadhi ya Wabunge kuna jambo wamekubaliana, na wanataka kutuletea mambo yasiyofaa ndani ya nchi yetu, na lengo lao kubwa ni kutetea mapenzi ya jinsia moja." amesema Kilakala.

"Napendekeza ikifika uchaguzi 2020, lazima kuna baadhi ya Wabunge wapimwe kabla hawajapewa fomu, namuomba Spika Ndugai kama ameweka vipimo, vya kuwapima baadhi ya Wabunge kuhusiana na ulevi pia aanze kuwachunguza wanaotajwa kujihusisha na mapenzi ya jinsia moja." amesema Kilakala.

Kwa sasa chama hicho kinafanya kampeni ya Kijani kwa ajili ya kujiandaa na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2020.