Alhamisi , 29th Aug , 2024

Wasanii wa maigizo nchini wameziomba Taasisi za Kibenki kupunguza masharti ya mikopo ili waweze kukopa kwa ajili ya kazi zao za Sanaa na kujikwamua kiuchumi.

Coletha Raymond, msanii wa maigizo.

Wanasema taasisi nyingi zinawataka watoe hati ya nyumba, shamba au kiwanja na wengi wao bado hawajafanikiwa kupata rasilimali hizo.
“Utakuta unaambiwa leta hati ya kiwanja, nyumba au shamba wakati mimi ndio kwanza najitafuta, wazo ninalo lakini namna ya kuluwezesha wazo langu liweze kuwa fedha ndio nahitaji fedha ili niweze kumiliki rasilimali wanazozihitaji kama dhamana”, alisema Francis Mushi, Msanii wa maigizo.
“Kwanza tutafutiwe soko halafu watupe mitaji kwa maana unaweza ukanipa mkopo natengeneza kazi lakini nikakosa wateja basi tuwekewe mifumo mizuri itakayotuwezesha kuuza bidhaa yetu ya sanaa”, alisema Coletha Raymond, Msanii wa maigizo.
Kwa upande wake mwenyekiti wa jukwaa hilo, Simon Jacob anaelezea umuhimu wa wasanii kuwezeshwa kiuchumi.
“Ukimuwezesha msanii unakuwa umewezesha nguvu kazi zote zinazofanyika kwenye uandaaji wa kazi za sanaa na tukiwezeshwa kichumi tunakuwa na uhakika wa kazi tunayoifanya iweze kufanyika kwa ubora”, alisema Simon Jacob.

Katibu mkuu wizara ya Utamaduni, Sanaa na michezo , Gerson Msigwa amezitaka taasisi za kifedha kuungana na wasanii kuwawezesha huku akitoa wito kwa wasanii kuwa waaminifu.
“Na nyie nao isije kuwa kukopa sherehe kulipa matanga, ukikopeshwa inabidi ukopesheke ujue na kulipa kwa maana unaweza kukopeshwa milioni 15 ukashindwa kulipa ukawakosesha wenzako waaminifu”, alisema Msigwa.