Alhamisi , 13th Sep , 2018

Serikali imepanga kukamilisha utaratibu mpya wa kuagiza sukari nchini ifikapo mwezi Oktoba mwaka huu. Utaratibu huo mpya unatagemewa kuwa mwarobaini wa kukomesha mlundikano wa sukari kwenye viwanda vya sukari nchini.

Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage.

Hakikisho hilo limetolewa leo Jijini Dodoma na Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage, wakati akiwasilisha taarifa ya hali ya sukari nchini.

Mh. Mwijage ameliambia Bunge kuwa sukari inayozalishwa nchini haikidhi mahitaji na kwa mwaka 2018/19 uzalishaji unakadiriwa kufikia tani 353,651 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na hakuna kiwanda kinachozalisha sukari kwa ajili ya matumizi ya viwandani.

Upungufu huo wa sukari inayozalishwa nchini umesababisha nakisi ya sukari takribani tani 316,349, tani 161,349 zikiwa za matumizi ya kawaida na tani 155,000 kwa ajili ya matumizi ya viwandani.

"Hadi kufikia Septemba 5, 2018, viwanda vyetu vilizalisha jumla ya tani 119,671.19 ambazo ni sawa na asilimia 33.84 ya malengo ya uzalishaji wa sukari kwa mwaka huu hivyo kiasi cha sukari kilichopo nchini kinatosheleza mahitaji ya sukari kwa kipindi cha miezi mitatu mbali na uzalishaji unaoendelea" amesema Waziri Mwijage.

Ili kulipatia ufumbuzi tatizo hilo Waziri Mwijage amesema, Serikali imeshatoa maelekezo kwa wamiliki wa viwanda vya sukari nchini kuwasilisha mapendekezo kuboresha mfumo wa usambazaji ili kuhakikisha upatikanaji wa bidhaa hiyo muhimu unakuwa wa uhakika na bei nafuu.

Akiongea kuhusu bei na upatikanaji wa sukari, amesema tathmini ya miezi sita kuanzia mwezi Machi hadi Agosti, 2018 inaonesha hali ya upatikanaji wa bidhaa hiyo ni mzuri na bei yake imekuwa ikitengemaa. kwenye tathmini hiyo ongezeko la bei limekuwa kati ya Shilingi 50 hadi Shilingi 150.

Mahitaji ya sukari nchini kwa mwaka yanakadiriwa kuwa tani 670,000 ambapo tani 515,000 ni matumizi ya kawaida na tani 155,000 ni kwa mtumizi ya viwandani.