Jumatano , 4th Oct , 2023

Serikali imeanza rasmi kutekeleza mkakati wa kuhakikisha bandari ya Mtwara inatumika katika kusafirisha zao la korosho na bidhaa nyingine za mazao kwa ajili ya kuuzwa nje ya nchi jambo litakaloinua uchumi wa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Naibu Waziri wa Uchukuzi David Kihenzile

Hayo yameelezwa leo Oktoba 4, 2023, na Naibu Waziri wa Uchukuzi David Kihenzile katika mkutano wa wadau wa zao la korosho kilichofanyika mkoani Mtwara kwa ajili ya maandalizi ya usafirishaji wa zao la hilo kupitia bandari ya Mtwara.

Waziri Kihenzile amesema baadhi ya hatua za utekelezaji zilizofikiwa na serikali katika kutekeleza agizo la Rais ni pamoja na kuundwa kwa kamati ya kutekeleza jambo hilo ikiongozwa na Naibu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari nchini (TPA) Mhandisi Juma Kijavara.

"Tumeshaanza kununua vifaa ikiwemo SSG moja kwa ajili ya kupakia na kushusha makasha,pia tunaenda kujenga kisiwa mgao ili bandari iwe na uwezo wa kuhudumia bidhaa kama vile saruji na makaa ya mawe," amesema Naibu Waziri Kihenzile.

Awali akizungumza katika mkutano huo Naibu Mkurugenzi Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari nchini (TPA) Mhandisi Juma Kijavara amesema bandari ya Mtwara imepiga hatua kiuwezo na kiutendaji ikilinganishwa na hapo awali kabla ya ujenzi wa gati mpya.

"Uwezo wa bandari yetu tangu ilipojengwa mwaka 1950 ilikuwa ni kuhudumia tani 400,000 lengo ambalo halikuwahi kufikiwa,lakini kwa mwaka uliopita imeweza kuhudumia tani milioni 1.6" Amesema Kajivala.

Muonekano wa bandari ya Mtwara

Aidha Naibu Waziri amesema kuwa ili kuondoa urasimu na usumbufu kwa wateja serikali inakusudia kuanzisha kituo cha pamoja(One stop center) ili kuhakikisha huduma zote zinapatikana kwa wakati.

Pia Naibu Waziri wa Uchukuzi ameiagiza TPA kusimamia ubora wa korosho inayosafirishwa ili kulinda uthabiti wa soko kwani vinginevyo itakuwa ni hasara kwa taifa.

Mkutano huo wa wadau wa korosho ni utekelezaji wa maagizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa alipofanya ziara mwezi uliopita katika mikoa ya Lindi na Mtwara ambapo aliagiza korosho kuanza kusafirishwa kwenda nje kwa ajili ya mauzo kupitia bandari hiyo.