Ijumaa , 19th Apr , 2024

Uongozi wa Yanga umeweka wazi kuwa watani zao wa jadi Simba wakijichanganya watawatuliza kimya kwa kuwa hesabu zao ni kupata matokeo kwenye mechi zote na sio dhidi ya Simba pekee.

Yanga watawakaribisha Simba kwenye mchezo wa Kariakoo Dabi unaotarajiwa kuchezwa Uwanja wa Mkapa Aprili 20 2024 wao wakiwa ni wenyeji wa mchezo huo.

Ipo wazi kwamba katika mchezo wa mzunguko wa kwanza uliochezwa Uwanja wa Mkapa baada ya dakika 90 ubao ulisoma Simba 1-5 Yanga.

Ali Kamwe, Ofisa Habari wa Yanga amesema kuwa wanatambua umuhimu wa kupata pointi tatu kwenye mechi ambazo wanacheza hivyo watani zao wa jadi wakijichanganya watakutana na kazi.

“Tunasikia kwamba wanahitaji kupata pointi tatu kwetu hilo tunalisikia lakini tunawaacha kwanza wakijichanganya tutawatuliza kimya kwa vitendo.

“Haupati ubingwa kwa ushindi wa mchezo mmoja Bali kwa kupata pointi tatu kwenye mechi zetu zote hivyo tupo tayari kwa mchezo mashabiki wawe tayari kushuhudia burudani,”.

Yanga ni vinara wa ligi na mkali wao wa kutupia ni Aziz KI mwenye mabao 14.