Alhamisi , 15th Oct , 2020

Mshambuliaji wa Manchester United, Marcus Rashford amekuja na kampeni mpya ya kutaka serikali ya Uingereza kuidhinisha ongezeko la bajeti ya huduma ya chakula kwa watoto mashuleni ili kupunguza baa la njaa miongoni mwao.

Mshambuliaji wa klabu ya Manchester United, Marcus Rashford (Pichani) akionesha makeke yake.

Huu ni mlolongo wa vitendo vya kiungwana kwa mchezaji huyo mara baada ya dunia kutambua mchango wake katika kusaidia kaya mbalimbali nchini Uingereza kwa kuwapa huduma mbalimbali ikiwemo chakula kipindi cha janga la ugonjwa wa COVID19.

Katika kampeni inayoendeshwa na mchezaji huyo mwenye miaka 22 ametaja mapendekezo matatu ambayo ni pamoja na ongezeko la idadi ya watoto milioni moja na laki tano wanaotakiwa wapate chakula ambao ni kuanzia wenye umri wa kati ya miaka 7 hadi 16.

Vilevile ongezeko la utoaji misaada hususani kipindi cha sikukuu kwa kutoa chakula kwa watoto na kuwasaidia shughuli zao mbalimbali hususani katika shule maalumu za watoto walio katika mfumo wa kupewa chakula cha bure kufikia watoto milioni moja na laki moja. Ongezeko la thamani ya bajeti ya afya kwa watoto kufikia paund 4.25 kwa wiki kutoka Paund 3.10 ya awali.