Jumapili , 23rd Aug , 2020

Wafanyabiashara wa Miwa katika soko la Tandale jijini Dar es Salaam wameiomba serikali kuwatengea eneo maalum ili kuondokana na adha wanayokutana nayo wanapoweka biashara hiyo barabarani.

Mzigo wa miwa ukiwa tayari umeshushwa kutoka kwenye gari la mizigo katika soko la Tandale.

Wakizungumza wa EATV wafanyabiashara hao wamesema kuwa kukosekana kwa eneo maalum la kupanga biashara zao kumepelekea hasara kwani miwa huharibika na hivyo kuongeza hasara na kusababisha kushindwa kurejesha mikopo yao kwa wakati.

Kwa upande wake Mjumbe wa wafanyabiashara wa Miwa, Hamis Abdallah amesema kuwa mazingira ya biashara yanahatarisha usalama wa maisha yao. “Eneo hili ni hatari sababu tupo barabarani kabisa, tunalazimika kukaa na madereva hadi mzigo utakapoisha ili kuhifadhi miwa kwenye gari”.

Rukia Kassim ambaye ni mfanyabiashara mwanamke anayejihusisha na biashara hiyo amesema kuwa ujenzi wa soko hilo utasaidia kuondoa msongamano katika eneo hilo ambao ni kero pia kwa wateja hivyo kuomba manispaa inayosimamia ujenzi huo kuweka mikakati ya upanuzi wa soko au kutenga aeno maalumu ili kuwasaidia kuendeleza biashara zao.