Ijumaa , 12th Sep , 2014

Wananchi wametakiwa kuwekeza katika elimu, kwani ndio njia pekee ya kuweza kujikwamua na umaskini kwa kuwa na idadi kubwa ya vijana waliosoma na wenye uwezo wa kufanya shughuli mbalimbali.

Mbunge wa Arumeru Magharibi, Godluck Ole Medeye (kushoto) akiteta jambo na waziri Mkuu Mizengo Pinda bungeni mjini Dodoma hivi karibuni.

Hayo yamesemwa jana na Mbunge wa Arumeru Magharibi , Godluck Ole Medeye wakati akizungumza katika harambee ya kuchangia bweni la wasichana la shule ya sekondari Lonange,Jijini Arusha ambapo jumla ya shilingi milioni 24 zimepatikana, huku kiasi kilicholengwa kuchangwa ni shilingi milioni 100.

Amesema swala la kuwekeza katika elimu linawahusu wadau mbalimbali pamoja na wazazi kwa ujumla, ili kuwezesha watoto waweze kuwa na shughuli za kufanya pindi wanakapohitimu masomo yao na kuondokana na changamoto ya ajira.

Medeye ameitaka jamii kuwa na mwamko katika kuchangia shughuli za maendeleo mashuleni, ikiwemo ujenzi wa mabweni na maabara, ili kuwawezesha wanafunzi kupata elimu iliyo bora na kuongeza kiwango cha ufaulu.