Alhamisi , 17th Mar , 2016

Waziri Kassim Majaliwa, amewasimamisha kazi watumishi wawili wa Halmashauri ya Wilaya ya Chato Mkoani Geita, kwa tuhuma za ubadhirifu, rushwa na matumizi mabaya ya madaraka.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akisalimiana na Mbunge wa Busanda, Lolesia Bukwimba baada ya kuwasili kwenye Ofisi yaMkurugenzi wa Wilaya ya Chato

Watumishi hao ni Mkuu wa Idara ya Kilimo na Ushirika, Bw. Mwita Mirumbe Waryuba pamoja na Afisa Maendeleo ya Jamii wa Wilaya, Bw. Dioniz Mutayoba.

Waziri Mkuu alitoa agizo hilo jana usiku alipokuwa akizungumza na watumishi wa idara zote na taasisi zilizomo kwenye wilaya ya Chato katika mkutano uliofanyika kwenye ukumbi wa Mshikamano SACCOS wilayani humo.

Afisa Kilimo na Ushirika anadaiwa kuchangisha kiasi cha sh. milioni 20 kutoka kwa watumishi wa Halmashauri hiyo kwa ajili ya kuanzisha SACCOS tangu mwaka 2013 lakini hadi sasa SACCOS haijaanzishwa na wala fedha hizo hazijarejeshwa. Fedha hizo zinadaiwa kuliwa na watumishi watatu (majina yamehifadhiwa).

Aidha, Bw. Waryuba anadaiwa kutumia lugha chafu na za vitisho kwa watumishi walio chini yake ikiwa ni pamoja na kuomba na kupokea rushwa, na kunyanyasa na kudhalilisha kijinsia baadhi ya watumishi wa kike.

Inadaiwa pia Bw. Waryuba alikopa bila kufuata taratibu za mikopo wilayani Chato ambapo alikopa sh. milioni 15 kutoka Mwambao SACCOS na sh. milioni 15 nyingine kutoka Chato Teachers’ SACCOS tangu mwaka 2015 na tangu wakati huo hajazirejesha hali ambayo imeleta manung’uniko kutoka kwa viongozi na wananchama wa SACCOS husika.

“Malalamiko ya watumishi na wananchi dhidi ya Afisa huyo yamefikishwa kwa Kaimu Mkurugenzi lakini hajachukua hatua kwa sababu ni rafiki yake,” alisema Waziri Mkuu. Kaimu Mkurugenzi huyo ni Mhandisi Joel Baha ambaye hakuwepo ukumbini hapo kwa sababu yuko kwenye ziara ya mafunzo huko Japan.

Kwa upande wake, Bw. Mutayoba ambaye ni Afisa Maendeleo ya Jamii wa wilaya hiyo anadaiwa kuzembea kusimamia mradi wa kufyatua matofali ya gharama nafuu (interlocking bricks) zilizogawiwa kwa vikundi vinne vya vijana wa wilaya hiyo.

“Mwaka 2013 Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) lilitoa mashine nne za kufyatulia matofali ya bei nafuu kwa ajili ya vikundi vinne vya vijana wilayani Chato. Mashine hizo ziligawiwa kupitia kwa Afisa Maendeleo ya Jamii wa wilaya, Bw. Dioniz Mutayoba na kila kikundi kilipewa sh. 500,000 ili waanze kazi ya kufyatua matofali na kuyauza kwa bei nafuu katika maeneo waliyopo lakini hadi leo hakuna kitu kilichofanyika,” inasema sehemu ya taarifa.

Afisa huyo anadaiwa kugawa mashine mbili kwa kila kata katika kata za Muganza na Buseresere lakini hadi sasa hakuna kilichofanyika kwani vikundi hivyo havikuzalisha kitu chochote tangu wakati huo.

Aidha, Bw. Mutayoba anatuhumiwa kudai na kupokea rushwa kwa wanachama wa vikundi vya ujasiriamali ili aweze kuvisaidia kupata mikopo. “Yaani watu wanakuja kukopa sh. milioni mbili halafu unawadai kitu kidogo cha sh. 300,000. Sasa mradi waliotaka kufanya wataweza kuukamilisha kweli?,” alihoji Waziri Mkuu.

“Huyu bwana amelalamikiwa lakini Mkurugenzi aliyepita lakini naye anadaiwa kumlinda kwa sababu ni rafiki yake,” alisema Waziri Mkuu na kuibua minong’ono ndani ya ukumbi huo. Aliyekuwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Chato, Bw. Clement Berege hivi sasa amehamishiwa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba.

“Katika Serikali hii tunataka tuwe na Halmashauri zilizo safi. Lakini pia Serikali hii ina mkakati wa kuimarisha ushirika na tunataka kuinua kilimo. Kwa hiyo basi, TAKUKURU na polisi wachunguzeni hawa watu wawili kwa maana ya Afisa Ushirika na Afisa Maendeleo ya Jamii na nipewe taarifa uchunguzi utakapokamilika,” alisema Waziri Mkuu.

Mapema, akizungumza na watumishi hao, Waziri Mkuu ambaye amewasili mkoani Geita kwa ziara ya siku mbili akitokea mkoani Kagera, alitumia fursa hiyo kuwakumbusha watumishi hao aliwakumbusha wajibu wao wa kuwahudumia Watanzania bila kujali hali zao na akasisitiza kuwa Serikali haitamuonea mtumishi yeyote ambaye anatimiza wajibu wake.

“Napenda kusisitiza kuwa malengo ya Serikali ni kuimarisha utendaji wa watumishi lakini pia Serikali hii haitamvumilia mtu mdanganyifu, mzembe, asiye mwadilifu na mla rushwa. Ukiharibu kazi hapa Chato mwwisho wako ni hapa hapa tu. Usitarajie kupelekwa Bunda au kwingine ili ukaharibu na huko,” aliongeza.