Alhamisi , 22nd Jan , 2015

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira, Ummy Mwalimu, ametoa miezi mitatu kwa viwanda vya A to Z na Sunflag vya jijini Arusha, kuacha kutumia magogo na kuni kwa ajili yakuendeshea viwanda hivyo.

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira, Ummy Mwalimu

Akizungumza jana jijini hapa, wakati wa ziara ya kutembelea viwanda hivyo, Naibu Waziri Ummy, amesema serikali inahitaji viwanda vizalishe bidhaa, lakini vinatakiwa kufuata sheria zote hususani sheria ya mazingira.

Amesema kutokana na hilo ni vema viwanda hivyo vikaacha kabisa kutumia magogo ya miti bila vificho kama wanavyofanya sasa.

Viwanda hivyo mbavyo awali vilikuwa vinatumia magogo katika kuendesha mitambo, kwa ajili yakuzalisha bidhaa na kwa sasa bado vinatumia kiasi kidogo cha kuni.

Aidha amesema kuwa endapo viwanda hivyo havitasitisha utumiaji wa kuni na magogo, katika kuendesha viwanda nchini, jitihada za serikali za kutunza mazingira hazitafanikiwa.

Pia Ummy ameomba wataalamu wa mazingira kushirikiana na uongozi wa A to Z, kufanya tathimini ya maji yanayotoka katika mitambo ya kiwanda hicho.

Mara baada ya Naibu Waziri kutoa maagizo hayo,baadhi ya wenye viwanda hivyo, wameahidi kutekeleza agizo hilo kwa kuacha kutumia kuni ifikapo mwezi Aprili.

Meneja Utumishi wa kiwanda cha Sunflag, Haroun Mahundi amesema, serikali iliwaagiza watumie makaa ya mawe katika kuendeshea viwanda vyao, jambo ambalo limekuwa na changamoto kubwa, japo wamefanikiwa utumiaji wa kuni kwa asilimia 75.