Jumatano , 25th Mei , 2016

Tanzania imekua miongoni mwa nchi chache katika bara la Afrika kufanikiwa kufikia lengo la nne la maendeleo ya millennia la kupunguza vifo vya watoto chini ya miaka mitano.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu,akihutubia mkutano wa 69 wa afya duniani unaoendela nchini Geneva-Uswisi.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu wakati akihutubia mkutano wa 69 wa afya duniani unaofanyika nchini Geneva, Uswisi.

Ummy alisema licha ya kukabiliwa na changamoto mbalimbali Tanzania imepiga hatua katika sekta ya afya kwa kupunguza vifo hivyo hadi kufikia vifo 54 kati ya vizazi hai 1,000 kutoka vifo 112 kati ya vizazi hai 1,000.

Aidha, mkutano huo ambao ni wa ngazi ya juu katika sekta ya afya duniani, Tanzania imetambuliwa na kutangazwa kuwa miongoni mwa nchi zilizotokomezwa ugonjwa wa polio kwa kufanikiwa katika utoaji wa huduma za chanjo nchini kwa watoto.

“Ninaeleza kwa masikitiko kuhusu tatizo la mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu uliopo nchini Tanzania ambapo hadi kufikia tarehe 22 Mei, 2016 idadi ya wagonjwa ilifikia 21,581,kati yao watu 338 wamepoteza maisha, naahidi Serikali kupitia wizara ya afya itaimarisha na kuzingatia kanuni za afya ya mazingira katika kukabiliana na ugonjwa huu, ” alisema Mhe. Ummy.

Kwa upande wa kutokomeza malaria Waziri Ummy alisema Tanzania imeweza kupunguza maambukizi ya ugonjwa huu kutoka asilimia 18 hadi 9.5 kwa Tanzania bara na kwa upande wa Zanzibar imefanikiwa kupunguza idadi ya wagonjwa hadi kufikia asilimia 0.6 .

Katika kuboresha huduma za afya nchini alisema Serikali ya Tanzania imejipanga na kuhakikisha itaboresha huduma za afya ziweze kumfikia kila mtanzania popote alipo, “ili kuweza kufikia malengo haya ni wakati muhimu sasa kuwekeza zaidi katika sekta hii kwa kuongeza uwekezaji katika raslimali fedha,watu pamoja na kuboresha miundombinu ikiwemo utoaji wa huduma za afya nchini”.

Waziri Ummy alisema katika kufikia mafanikio ,wizara ya afya inatarajia kuwasilisha muswada wa sheria katika bunge la mwezi wa Septemba,2016 wa kila mtanzania kuwa na bima ya afya kitu ambacho kitakuwa ni mkombozi mkubwa kwa mwananchi katika kupata huduma za matibabu wakati wowote anapokuwa na fedha au kutokuwa na fedha kwa kuwa maradhi hayachagui wakati.

Mkutano mkuu wa mwaka wa Afya Duniani hufanyika nchini Geneva –Uswis kila mwaka mwezi mei ambao huwakutanisha mawaziri wa afya kutoka nchi wanachama wa Shirika la afya Duniani {WHO} na kuhudhuriwa na wadau,mashirika na taasisi zinazoshiriki katika kutoa huduma za afya Duniani.Tanzania inawakilishwa na waziri wa afya Tanzania bara Mhe.Ummy mwalimu na Waziri wa Afya Zanzibar Mhe. Mahmoud Kombo.