Ijumaa , 1st Aug , 2014

Serikali ya Tanzania imesema imeweka mikakati ya kupambana na ugonjwa wa ebola ambao umeua watu 729 katika nchi zilizokumbwa na ugonjwa huo Afrika Magharibi.

Msemaji wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii Nsachris Mwamwaja (katikati) akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa Idara ya Habari Maelezo.

Akiongea leo jijini Dar es salaam msemaji wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii nchini Bw. Nsacris Mwamwaja amesema serikali imejiandaa kusambaza vifaa vya kinga kwa watumishi wa afya ikiwa ni pamoja na ufatiliaji katika maeneo ya mipakani, bandarini na kwenye viwanja vya ndege.

Mwamwaja amesema mpaka sasa hakuna taarifa za kuingia kwa ugonjwa huo hapa nchini ambapo amewataka wananchi kuchukua tahadhari
stahiki kwa kuwaona wataalamu wa afya mara wanapohisi kuwa na dalili za ugonjwa huo kwa kuwa ugonjwa huo huambukizwa.

Wakati huo huo, idadi ya watoto wanaokufa kwa ugonjwa wa saratani katika hosptali ya Muhimbili jijini Dar es salaam nchini Tanzania imepungua mara baada ya kujengwa wodi ya watoto wa ugonjwa huo.

Akiongea leo jijini Dar es salaam mmoja wa waliochangia ujenzi wa wodi hiyo August 2013, Zainul Dosa amesema idadi ya vifo imepungua kutoka asilimia 85 mpaka 35 kwa wagonjwa wanaofika katika hospital hiyo.

Dosa amesema idadi ya vifo imepungua kutokana na kiwango cha maambukizi kwa watoto hao kuwekwa katika mazingira yanayoepusha kuambukizana saratani na hivyo kuwataka watanzania kusaidia kujenda utamaduni wa kusaidia katika upatikanaji wa huduma bora za afya.