Alhamisi , 7th Apr , 2016

Waziri wa Afya , Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu, amezindua kampeni ya mzee kwanza yenye lengo la kuwatahmini wazee kwa kuwapatia kipaumbele katika huduma stahiki hususani Afya.

Waziri wa Afya , Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu,

Akizungumza katika uzinduzi huo ambao umefanyika kitaifa mkoani Morogoro Mhe. Ummy Mwalimu amesema serikali imeandaa mswada wa sheria ya wazee ambapo utapelekwa bungeni ili upitishwe kuwa sheria ambayo itasimamia upatikanaji wa haki na ustawi wa wazee nchini.

Mhe. Ummy ameongeza kuwa sheria hiyo itatoa ahueni kubwa kwa wazee na kuboresha sana maisha yao ambapo amesema kuwa mwezi wa tisa wamepanga kuufikisha rasmi bungeni kwa ajili ya kufanyiwa kazi.

Aidha Waziri huyo wa Afya amesema takwimu zinaonyesha jumla ya wazee wote nchini wanaopata huduma ya Pensheni na NHIF ni sawa na asilimia 4 tu ya wazee wote nchini huku bima ya Afya ikihudumia wazee 52,000 tu.

Ameongeza kuwa hatua kubwa ambayo serikali imeshachukua mpaka sasa ni kuagiza kila halmashauri nchini ni kubainia wazee waliokatika maeneo yao na kuhakikisha wanapata huduma zote za msingi kutoka kwenye mapato yao ya ndani.

Aidha Mhe Ummy amewaagiza viongozi wote wa halmashauri zote nchini wahakikishe kuwa wanatoa vibali vya matibabu bure ikiwepo kutoa vipimo vya magonjwa yote bure kwa wazee wote katika maeneo yao.