Jumatano , 8th Jun , 2016

Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa, amezindua mpango wa maendeleo wa miaka mitano na kusema kuwa serikali ya awamu ya tano imejipanga kufufua viwanda vilivyokufa pamoja na kulifufua shirika la ndege la Tanzania kwa kununua ndege mpya.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizindua Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2016/17-2020/21 kwenye Ukumbi wa Chuo cha Mipango mkoani Dodoma.

Mhe. Majaliwa ametoa kauli hiyo jana mjini Dodoma kwenye uzinduzi wa mpango wa maendeleo wa Taifa wa miaka mitano 2016/2017 hadi 2020/2021 uzinduzi uliofanyika kwenye chuo cha mipango na maendeleo vijijini.

Aidha, Mhe. Majaliwa amesema kuwa serikali itaanza ujenzi wa reli ya kati kuanzia jijini Dar es Salaam hadi Mkoani Mwanza pamoja na matawi yake kwa kiwango cha standard gauge ili kuharakisha maendeleo kwa wananchi.

Katika taarifa yake kuhusu uzinduzi wa mpango huo Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dk. Philip Mpango amesema lengo la kuanzisha mpango huo ni kutekeleza adhima ya dira ya taifa ya maendeleo kufikia uchumi wa kati.

Amesema serikali inatarajia kufufua miradi mikubwa ambayo ni kichocheo cha maendeleo ya Taifa ikiwemo kufufua viwanda mijini na vijijini ili kuwawezesha Watanzania kuwekeza katika miradi ya maendeleo.