Jumatano , 24th Jun , 2015

Mbunge wa jimbo la Arusha Mjini, Godbless Lema, (CHADEMA), amemtaka Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas, kujiandaa kupokea mkanda wa DVD ya bomu lililorushwa katika mkutano wa CHADEMA, Juni 15, 2013 kabla ya Bunge kuvunjwa.

Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, Godbless Lema, (Chadema).

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake leo, Lema amedai amechukua hatua hiyo, kutokana na Kamanda Sabas kutuma jopo la polisi toka nje ya Arusha kuja jijini hapa kwa ajili ya kazi maalum ya kumvunja miguu Lema kabla ya uchaguzi kuanza.

Amesema umma wa Watanzania anapenda wajionee magaidi wa jeshi la polisi waliohusika kufanya unyama katika ufungaji wa kampeni za udiwani kwenye mkutano wa hadhara wa CHADEMA na waunganishwe na magaidi waliowakamata.

Lema amesema atapenda mkanda huo amkabidhi Sabas bungeni, kabla halijaisha ili umma uwaone magaidi wa jeshi la polisi waliohusika katika tukio hilo na waunganishwe pamoja na magaidi wenzao waliokamatwa.

Kuhusu uandikishwaji amesema Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) inafanya hujuma ya kukatiza uandikishwaji wakati idadi ya watu ikiwa kubwa kwenye kata zilizoanza kuandikisha.

Amesema Tume wanachofanya ni kuorodhesha majina ya watu waliokuwepo juzi Juni 22 kituoni na Juni 23 wanawamalizia hao na wanaokuja ambao ni wengi wanakataliwa kuwa zoezi limefika mwisho maeneo hayo, wakati maeneo mengi wameongeza siku tatu na siyo majiji makubwa kama Arusha.

Amesema tayari ameagiza wenyeviti wa mitaa kukusanya idadi ya wapiga kura waliobaki kila mtaa na walioandikishwa, kasha atafanya maandamano makubwa ya kupinga dhambi hiyo.

Hata hivyo, amemwomba Rais Jakaya Kikwete kumwondoa Jaji mstaafu, Damian Lubuva, katika nafasi hiyo, kutokana na kushindwa kuendesha vizuri kazi ya uandikishwaji na kuhatarisha amani ya Tanzania katika uchaguzi ujao.