Jumatano , 13th Jan , 2016

Mama mmoja Mkoani Dodoma anatuhumiwa kumuozesha mtoto wake mwenye umri wa miaka 13 (jina linahifadhiwa) kwa mahari ya shilingi laki sita pamoja na ng’ombe wanne.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu

Tukio hilo lilitokea jana katika Mtaa wa Chikole, Kata ya Msalato katika Manispaa ya Dodoma ambapo mama huyo aliyefahamika kwa jina la Melea Mazengo ameamua kumuozesha binti yake huyo kwa kijana mmoja aliyefahamika kwa jina moja la Juma ambaye naye ni mkazi wa mtaa huo.

Hata hivyo mpango huo wa ndoa ulitibuliwa na mwenyekiti wa mtaa huo, Nashoni Chinywa ambaye baada ya kupata taarifa za ndoa hiyo aliamua kuita polisi ili kuivunja.

Akizungumzia tukio hilo mama mzazi wa mtoto huyo, Mdala Mazengo amesema kuwa aliamua kumuozesha binti yake baada ya binti huyo kumtaarifu kuwa amepata mchumba.

Kwa upande wa binti huyo amesema kuwa alikutana na kijana huyo Juma (20) na kumwambia kuwa anampenda lakini yeye aliona kuwa anamtania na kuamua kuachana naye.

Hata hivyo baadhi ya majirani wa mama huyo wamesema kuwa ni tabia ya mama huyo ambaye ni mjane kuwaozesha watoto wake wakiwa katika umri mdogo kwani kuna mwanaye mmoja mwenye umri wa miaka 14 alibebeshwa mimba na mpaka sasa ana mtoto mdogo anayemlea.

Naye mwenyekiti wa mtaa huo, Nashoni Chinywa amesema kuwa baada ya mahojiano mama huyo alikiri kosa lake na kusema kuwa amechochwa na malezi ya watoto hao kwani hata dada yake mwenye umri wa miaka 14 alibebeshwa mimba akiwa nyumbani hivyo akaona ni bora amuozeshe na huyo mdogo wake ili asije akabeba mimba nyumbani