Wednesday , 16th Oct , 2024

Wizara ya mifugo na Uvuvi imeagizwa kushirikiana na sekta binafsi kwa ajili ya kuandaa mashamba darasa kwa ajili ya uzalishaji wa kuku wazazi, wa mayai, nyama na vifaranga ili kuongeza uzalishaji utakaopunguza changamoto ya mahitaji ya nyama hiyo.

Dkt.Doto Biteko, Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati

Agizo hilo limetolewa na Naibu Waziri Mkuu, Dokta Doto Biteko wakati anafungua kongamano la ufugaji wa kuku na ndege warukao kwa nchi za kusini mwa Afrika leo jijini Dar es Salaam.

“Niwaagize wizara ya mifugo na uvuvi kushirikiana sekta binafsi muanzishe mashamba darasa kwa ajili ya kuku wazazi, kuku wa nyama na kuku wa mayai, na kuku vifaranga kwa ajili kuongeza uzalishaji”, Dkt. Doto Biteko, Naibu Waziri Mkuu.

Kwa upande wake waziri wa Mifugo na uvuvi Abdallah Ulega amewataka watafiti wa vyakula Vya mifugo kuzingatia taarifa za chunguzi zao kwa kuzingatia maslahi ya Taifa.

“Pindi mnapofanya tafiti ni vizuri kueleza majibu ya tafiti pamoja na mkakati usioleta taharuki katika jamii katika ulishaji wa kuku, kwa sababu mnapofanya tafiti na kutoa majibu ya tafiti bila kuangalia madhara yake mnazua taharuki ambazo zinarudisha nyuma juhudi kubwa za Serikali zinazofanya kwenye uwekezaji wa ufugaji na kusababisha watu kuogopa kula nyama za kuku kwa ajili ya wafugaji wachache wanaofanya vitu visivyofaa”, Abdallah Ulega, Waziri wa Mifugo na Uvuvi.

Mkurugenzi Mkazi wa shirika la uboreshaji wa kijana Tanzania (Agra) Vianey Rweyendela anaelezea umuhimu wa kongamano hilo huku baadhi ya wafugaji wakitoa maoni yao ili kuchochea ufugaji wa kuku nchini.
“Tunawajengea uwezo wa kifedha, tunawaongezea tija ya mkulima ili kuongeza thamani ya bidhaa yake inapofika sokoni iweze kuwa na thamani”, Vianey Rweyendela, Mkurugenzi Mkazi AGRA.
“Tunafanya ufugaji wa jadi tunaomba Serikali ituwezeshe tuweze kufanya ufugaji wa tija ili wafugaji waweze kufuga kwa kuboresha uchumi wao”, Omary Musa, Mfugaji wa Kuku.
“Kwanza watoe Elimu lakini pia watuwezeshe kifedha na miundombinu ili tuweze kuongeza uzalishaji na tuweze kutumia sadc corridor kuwalisha nchi ambazo Zina uhaba mkubwa wa nyama ya kuku”, Grace Urassa, Mfugaji wa Kuku.