Thursday , 22nd Aug , 2024

Watanzania wametakiwa kuhifadhi chakula kuelekea katika msimu wa mvua za Vuli 2024 kwani kutakuwa na upungufu wa uzalishaji mazao kutokana na kuwa na Mvua za wastani na chini ya wastani.

Dkt. Ladislaus Chang'a, Kaimu Mkurugenzi Mkuu TMA.

Tahadhari hiyo imetolewa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya hewa nchini(TMA), wakati anatoa ripoti kwa wanahabari kuelekelea msimu huo unaotarajiwa kuanza mwishoni mwa Septemba mpaka Disemba 2024.
“Tunashauri wananchi wahifadhi chakula cha kutosha kwa maana msimu huu kutokana na upungufu wa unyevunyevu ardhini ambao utaathiri shunguli za Kilimo na malisho ya wanyama, hivyo tunawashauri wakulima kuchagua mazao ambayo yanahimili changamoto hii ya hali ya hewa”, alisema Dkt. Ladislaus Chang'a, Kaimu Mkurugenzi Mkuu TMA.

Mtaalam wa hali ya Hewa (TMA) anaelezea mafanikio ya tathmini ya utabiri wa mvua za Masika 2024.
“Kutokana na Mvua za Masika zilizoanza kunyesha Machi mpaka Mei 2024, ni sawasawa na tulivyotabiri hivyo utabiri unaofanywa na TMA ni sahihi kwahiyo wananchi wachukue tahadhari kwa kadri ya tabiri zetu tunavyozitoa”, alisema  Alfred Kondowe, Mtaalam wa Hali ya Hewa (TMA).

Kwa upande wao wananchi waiomba Serikali kuweka mifumo imara itakayozuia baa la njaa.
"Naishauri Serikali izuie mipakani na kuhifadhi chakula cha kutosha ili inapotokea msimu wa upungufu wa chakula kusiwe na baa la njaa ambalo linaweza kuepukika", alisema Hamis Ngeta, Mkazi wa Dar es Salaam.

"Kuna wakulima wengi sana nchini lakini hawana mashamba ya kulimia kwahiyo wakiwezesha kwenye yale maeneo ambayo hayatumiki yatasaidia kuzalisha chakula cha dharura kuelekea msimu huo", alisema Hassan Hamis, Mkazi wa Dar es Salaam.