Friday , 9th Aug , 2024

Mabinti rika balehe mkoani Kagera wametakiwa kujishughulisha na ujasiriamali hali itakayowawezesha kujitegemea na kuepukana na vitendo vya kujihusisha na ngono zembe inayoweza kupelekea kupata maambukizi mapya ya virusi vya UKIMWI.

Mwendesha warsha hiyo ya siku moja Peter Kilima

Akizungumza na EATV mara baada ya mafunzo ya uwasilishaji mada ya ujasiriamali, mwendesha warsha hiyo ya siku moja Peter Kilima amesema kuwa jumla ya washiriki 30 wamenufaika na mafunzo hayo.

Aidha ameongeza kuwa lengo la mafunzo hiyo ni kuwasaidia kuanzisha miradi mbalimbali ya kiuchumi na kusimamia miradi waliyonayo kwa lengo la kupata faida na kuepukana na kupata maambukizi ya virusi vya UKIMWI.

Jaquelin Peter na Davida Deogratius ni miongoni mwa mabinti rika balehe 30 waliopata elimu ya ujasiliamani ambapo wamesema kuwa elimu hiyo imewapa mwanga bora wa kuwa wajasiriamali wa kujitegemea na kuepukana na vishawishi vya kujihusisha na ngono zembe.

Mafunzo hayo yametolewa na Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo - SIDO kwa kushirikiana na Shirika la MDH katika kituo cha SIDO Dream Centre kilichopo kata ya Rwamishenye Manispaa ya Bukoba mkoani Kagera.