Tuesday , 9th Jul , 2024

Wananchi katika kata ya Luchelele jijini Mwanza kwa kushirikiana na Jeshi la polisi mkoani humo wamewezesha kubaini uwepo wa usafirishaji wa siri wa mifuko ya Plastiki zaidi ya magunia 80 yenye jumla ya mifuko milioni 11.

Taarifa za usafirishaji wa mifuko hiyo na kuletwa katika eneo mojawapo lilipo katika kata ya Luchelele zimetolewa na wasamalia wema na kuwezesha jeshi la polisi mkoani humo kufika mapema na kukamata mifuko hiyo pamoja na baadhi ya watuhumiwa.

Diwani wa kata ya Luchelele anaeleza namna ushirikishwaji wa jamii katika masuala ya usalama ulivyowezesha kutolewa kwa taarifa hizo kwa wakati.

Kamanda wa jeshi la Polisi mkoani Mwanza Wilbroad Mutafungwa amesema wamewashikiria watuhumiwa watatu huku akiwataka waliokimbia kujisalimisha mara moja.

Kwa upande wake meneja wa kanda wa Baraza la hifadhi na usimamizi wa Mazingira emewataka wafanyabiashara kuachana na matumizi ya mifuko hiyo ya Plastiki ili kuepusha madhara mbalimbali ya Mazingira.