Saturday , 10th Feb , 2024

BOHARI ya Dawa MSD imetunukiwa tuzo katika mkutano wa kimataifa wa magonjwa ya moyo. Tuzo hiyo ilikabidhiwa na Makamu wa Rais Dk Philip Mpango.

Tuzo hiyo imetolewa na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), kwa kutambua mchango wa MSD katika kuhakikisha bidhaa za afya zinahusisha upatikanaji wa huduma, dawa na vipimo vya magonjwa ya moyo.

Tuzo hiyo imetolewa baada ya ufunguzi wa mkutano wa madaktari wa moyo Afrika na Dk Mpango ambapo amesema mchango wa taasisi hizo za afya katika mapambano ya ugonjwa wa moyo ni kubwa ambapo zinaungwa mkono na serikali.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa (MSD) ambao ni moja ya wadhamini wa mkutano alisema,  JKCI ni moja ya wateja wakubwa wa bohari hiyo.

“JKCI ni moja ya wateja wetu wakubwa ambao hawana deni na tunashirikiana katika kuhakikisha tunamsaidia Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kuboresha sekta ya afya kwa Watanzania kwa kuwa na huduma bora,”alisema.

Alisema, taasisi hiyo imekuwa ni wadau wakubwa kwa MSD ambao wanatoa oda ya mahitaji yao kwa wakati na yaliyo na maoteo sahihi na wamekuwa wakihakikisha wanatujengea uwezo, kupata wazabuni, kujifunza teknolojia mpya, kununua bidhaa na vifaa vyenye uhitaji.

Naye Meneja wa MSD Kanda ya Dar es Salaam Betie Kaema alisema, lengo la kushiriki mkutano huo ni kutanua wigo kwa wataalamu wa magonjwa ya moyo Afrika kutambua uwezo wa MSD katika kuhudumia sekta hiyo.

“MSD kwa sasa imejikita zaidi katika upatikanaji wa dawa, vifaa na vitendanishi kwa ajili ya uchunguzi na tiba kwa ajili ya ugonjwa wa moyo, tuko hapa kuelekea mazuri yanayofanywa na serikali yetu kupanua wigo wa huduma,”alisema.