Friday , 11th Aug , 2023

Jeshi la Polisi Tanzania, limetoa onyo kali watu wanaotangaza mpango wa kuiangusha serikali ya awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan likibainisha kuwa huu ni uhaini na hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.

Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini IGP Camillus Wambura

Akitoa taarifa hiyo, Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini IGP Camillus Wambura ameeleza kuwa taarifa hiyo imekuwa ikisambaa tanga jana Agosti 10, 2023 kwenye mitandao ya kijamii ikihusu kundi la watu ambao wameeleza kwamba wanaandaa maandamano ya nchi nzima ili kuiangusha serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya awamu ya sita kabla ya mwaka 2025 huku hoja inayotajwa ikihusu masuala ya bandari.

“Kumekuwa na taarifa ikisambaa tanga jana Agosti 10, 2023 kwenye mitandao ya kijamii ikihusu kundi la watu ambao wameeleza kwamba wanaandaa maandamano ya nchi nzima ili kuiangusha serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya awamu ya sita kabla ya mwaka 2025” – amesema IGP Wambura

Aidha IGP ametaka wananchi kuzipuuza taarifa hizo zitakazoiingiza nchi kwenye machafuko, huku akiahidi kuwa Jeshi la Polisi halitakaa kimya katika hili, na hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya makosa hayo ya uchochezi.

“Jeshi la polisi halitakaa kimya na kuwavumilia, kama walidhani tuko kimya basi tutakwenda kuwaonyesha hatuko kimya kwa yeyote atakayevunja sheria za nchi, wasitikise kiberiti” -amesema IGP Wambura

Jeshi la Polisi Tanzania limetaka mambo ya kisiasa yaendelee kwa hoja za kisiasa na yasiingie kwenye matendo yoyote ya kihalifu.