Wednesday , 21st Oct , 2020

Klabu ya Mbeya City imetangaza kusitisha rasmi mkataba wa kazi na mwalimu Amry Said Juma kama kocha mkuu wa timu hiyo yenye maskani yake jijini Mbeya.

Kocha Amry Said aliyefutwa kazi ya kikonoa kikosi cha Mbeya City.

Katibu Mkuu wa Klabu hiyo Emmanuel Kimbe amesema maamuzi hayo yamefikiwa baina ya pande mbili baada ya majadiliano kutokana na mwenendo usioridhisha wa timu hiyo inayoshiriki katika ligi kuu inayoendelea.

Amry Said alijiunga na Mbeya City Disemba mwaka jana katika mzunguko wa pili wa michezo ya ligi Kuu 2019/2020.

Licha ya kuinusuru timu hiyo kushuka daraja, Amry amekua na wakati mgumu kwakuwa katika mechi saba za VPL amepoteza mara tano na sare mbili.

Katika kipindi hiki cha mpito timu itakuwa chini ya kocha msaidizi Mathias Wandiba na uongozi unaendelea kufanya jitihada za kusaka mrithi wa Amry Said mpaka atakapopatikana.

Kuondoka kwa Amry Said kunafikisha idadi ya makocha wanne walioachana na vilabu vya VPL tangu kuanza kwa msimu wa 2020/21, ambapo mapema Yanga ilimuondoka Zlatko Krmpotic, Ihefu iliachana na Maka Mwalwisi nayo Mtibwa ilitangaza kujiuzulu kwa aliyekua kocha wake Zuberi Katwila aliyetimkia Ihefu.