
Mgombea urais kupitia CHADEMA, Tundu Lissu.
Lissu ametoa kauli hiyo hii leo Septemba 30, 2020, wakati akizungumza na waandishi wa habari mkoani Arusha, na na kusisitiza kuwa kwa sababu hana wito wowote yeye ataendelea na ratiba zake za kampeni kama ilivyo kwenye ratiba.
"Kama kweli mimi ni mlalamikiwa, kanuni za maadili zinasema mlalamikiwa aandikiwe malalamiko na akabidhiwe na yeye ndiye anayetakiwa kuitwa, hadi hapa niliposimama tangu mmeanza kusikia mimi kuitwa kwenye kamati ya maadili, sijaona afisa yoyote wa tume akinifuata kuniletea malalamiko yoyote kwa maandishi na wito wowote,” alisema Lissu.
Aidha, Lissu amedai kwamba Watanzania wapo tayari kuipigia kura CHADEMA kwenye nafasi ya urais, ubunge na udiwani na kila mahali ambako amekwenda amepokelewa na amehutubia mikutano ya maelfu ya Watanzania na kati yao hakuna hata mmoja aliyehitaji kuhongwa.
Jana Septemba 29, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC Dkt. Wilson Mahera alitoa taarifa ya kuthibitisha kumuandikia barua ya wito Tundu Lissu, kufuatia tuhuma mbalimbali anazodaiwa kuzitoa kati ya Septemba 25 na 26 mjini Musoma dhidi ya NEC na mgombea urais kupitia CCM Dkt John Magufuli.