Friday , 13th Mar , 2020

Aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa BAVICHA, Patrick Ole Sosopi, amesema tayari imekwishatumwa timu ya Mawakili katika kituo cha Polisi cha Sitakishari wanakoshikiliwa Wabunge Ester Bulaya, Halima Mdee, Meya wa Ubungo Boniface Jacob na wanachama wengine na kudai kwamba wamejeruhiwa kwa kipigo.

Mbunge Halima Mdee, Meya wa Ubungo Boniface Jacob, Mbunge Ester Bulaya.

Akizungumza na EATV&EA Radio Digital leo Machi 13, 2020, Sosopi amesema kuwa hadi sasa hawajaelezwa sababu ya kushikiliwa kwa viongozi hao na kwamba Mawakili watakapowasili watafanya utaratibu wa kuwapeleka waliojeruhiwa hospitali kwa ajili ya matibabu.

"Mpaka sasa hatujaambiwa sababu ya wao kukamatwa, na taarifa tuliyonayo ni kwamba wamepigwa sana wako majeruhi na sasa Mawakili wetu kutoka Makao Makuu ya chama wameelekea Sitakishari kwa ajili ya kwenda kujua hali zao na ikiwezekana basi tuweze kupata nafasi za hao majeruhi kwenda kupata matibabu" amesema Sosopi.

Mdee na wenzake wamekamatwa leo mchana maeneo ya Segerea, walikoenda kwa ajili ya kumpokea Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa Freeman Mbowe, baada ya kulipiwa faini yake ya Milioni 70.