Tuesday , 24th Sep , 2019

Afisa Habari mpya wa Klabu ya Yanga, Hassan Bumbuli amesema kuwa hajaingia kwenye nafasi hiyo kwa ajili ya kuingia kwenye malumbano na Msemaji wa Klabu ya Simba Haji Manara, badala yake amekuja kufanya majukumu yake kitaaluma.

Bumbuli ametoa kauli hiyo wakati akizungumza kwenye kipindi cha KipengaXtra kinachoruka kila siku ya Jumatatu hadi Ijumaa kupitia East Africa Radio, kuanzia saa 6 kamili Mchana.

Amesema kuwa Yanga haihitaji mtu wa aina ya Haji Manara kwakuwa vitu vya kitaaluma haviwezi kuchanganywa na siasa, "ukisema Yanga itaifunga Barcelona hapo utashangaza ulimwengu, huwezi kuwaaminisha watu kitu kisichowezekana kama ukiwa mwanataaluma."

Bumbuli ameongeza akisema, "mimi kuwepo Yanga ni mafanikio makubwa sana kwa sababu nitafanya kile ambacho nilikusudia ndani ya Yanga na ilikuja baada ya kuona kuna tatizo la uongozi, nikaamini kwa pamoja tutaikomboa."

Hivi karibuni uongozi wa Yanga ulimtangaza Hassan Bumbuli kuwa Afisa Habari mpya wa Klabu hiyo huku nafasi ya Afisa Uhamasishaji ikienda kwa Antonio Nugaz.