Thursday , 13th Dec , 2018

Kwa mujibu wa ripoti, klabu ya Yanga imemalizana na kiungo wa  zamani wa Simba ambaye anakipiga na African Lyon, Haruna Moshi 'Boban' kwa kumpa mkataba wa kuitumikia klabu hiyo hadi mwisho wa msimu.

Kushoto ni Haruna Moshi akisaini mkataba mbele ya Mwenyekiti wa kamati ya usajili ya Yanga Hussein Nyika.

Haruna Moshi 'Boban' amesaini mkataba wa miezi sita kuitumikia klabu hiyo na kumaliza tetesi za muda mrefu juu ya hatma ya mchezaji huyo. Boban amejiunga na Yanga baada ya kuwa na msimu mzuri katika kikosi cha African Lyon akiwa ameifungia mabao mawili katika Ligi Kuu.

Inaelezwa kuwa usajili huo ni kutokana ana pendekezo la kocha mkuu wa Yanga, Mwinyi Zahera katika eneo la kiungo. Boban aliwahi kuzichezea Simba, Mbeya City, Friends Rangers na IF Gefle ya Sweden.

Kumekuwa na taarifa siku za karibuni za Yanga kuhitaji saini ya mkongwe huyo, ambapo kwa nyakati tofauti kocha wa Yanga, Mwinyi Zahera na Afisa Habari wake, Dismas Ten wamethibitisha ubora wake na kusema kwamba siku si nyingi watatangaza rasmi kama watamsajili au la.