Tuesday , 22nd Nov , 2016

Juhudi za serikali za kujenga uchumi wa viwanda zinaendelea kuungwa mkono na wadau wa ndani na nje ya nchi baada ya Shirika la Maendeleo la Ufaransa AFD hii leo kusaini makubaliano yaliyowezesha upatikanaji wa shilingi za Tanzania bilioni 25.67.

Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania Bi. Malika Berak (katikati) akishuhudia makabidhiano ya mkataba wa utolewaji wa pesa kwa ajili ya miradi ya nishati mbadala

Pesa hizo ni kwa ajili ya kusaidia uwekezaji kwenye nishati mbadala na ufanisi katika matumizi ya nishati.

Balozi wa Ufaransa nchini Bi. Malika Berak ndiye aliyekuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo ambapo amesema kiasi hicho cha pesa kitatumika kwa ajili ya mikopo ya gharama nafuu kwa miradi ya nishati mbadala kupitia benki ya BOA.

Moja ya wanufaikia wakubwa wa pesa hizo ni wamiliki wa viwanda vidogo, vikubwa na vya kati ambao ni wanachama wa Shirikisho la Wenye Viwanda nchini CTI kama anavyoeleza Mratibu wa Matumizi Bora ya Nishati wa CTI Bw. Thomas Richard.

Balozi Malika kwa upande wake amesema kutolewa kwa pesa hizo ni sehemu ya utekelezaji wa Azimio la Mazingira la Paris ambapo nchi mbalimbali duniani zimekubaliana kuwa na vyanzo vya nishati ambavyo ni rafiki kwa mazingira.