Thursday , 21st Jan , 2016

Shirikisho la Soka Nchini TFF limekubaliana na uamuzi wa Kamati ya Maadili ya Chama cha Mpira wa Miguu cha Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) wa kuwasimamisha kwa muda wa miaka miwili viongozi watatu wa Chama cha Mpira wa Miguu cha Wilaya ya Temeke TEFA.

Katibu wa TFF Mwesigwa Celestine amesema, kufungiwa kwa viongozi hao kunatokana na muenendo mzima wa uchaguzi Mkuu wa viongozi wa TEFA uliofanyika Novemba 22 mwaka jana ambapo mdau wa Soka wilayani humo alifungua kesi kuhusiana na viongozi wa TEFA.

Mwesingwa amesema, mdau huyo aliyejulikana kwa jina la Sudi Malilo alifungua kesi mbili ikiwa ya shauri la ombi la kuwasimamisha kwa muda viongozi wa TEFA pamoja na kesi ya msingi ambapo alihoji mwenendo mzima wa uchaguzi wa TEFA na uhalali wa viongozi waliochaguliwa ambapo shauri hili liliitaka Mahakama ikibaini kasoro za kisheria ibatilishe mchakato mzima wa uchaguzi na kuwaondoa madarakani viongozi waliochaguliwa.

Mwesigwa amesema, washtaki na washtakiwa wote wakiwemo TFF, DRFA na TEFA hawatatakiwa kuchuakua hatua zozote kuhusu uchaguzi wa TEFA pamoja na viongozi wake hadi kesi hiyo itakapokuwa imekwisha au mahakama kutoa amri yoyote kuhusu uchaguzi na viongozi wake.