Tuesday , 6th May , 2014

Rais wa zamani wa TFF Leodgar Tenga ameteuliwa kuwa mwenyekiti wa mfuko maalum wa maendeleo ya soka utakaoanzishwa hivi karibuni na shirikio la soka Tanzania TFF.

Rais wa zamani wa TFF Leodgar Tenga

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limeazimia kuanzisha Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu Tanzania (TFF Development Trust Fund).

Uamuzi wa kuanzisha mfuko huo umepitishwa katika kikao cha Kamati ya Utendaji ya TFF iliyokutana Mei 3 mwaka huu jijini Dar es Salaam ambapo madhumuni yake ni kutafuta vyanzo vya rasilimali za kuendeleza programu za mpira wa miguu Tanzania.

Mfuko huo utakaokuwa chini ya uenyekiti wa Rais aliyepita wa TFF, Leodegar Tenga utatafuta rasilimali za kuendeshea michuano ya Taifa na kimataifa ya wavulana na wasichana kwa vijana wenye umri chini ya miaka 13, 15, 17 na 19.

Pia kuendeleza maeneo ya ardhi kote Tanzania ambayo ni mali ya TFF kwa kujenga vituo vya michezo (sports centres), kutafuta rasilimali za kutoa mafunzo kwa makocha, marefa, madaktari wa tiba ya michezo na viongozi (administrators).

Majukumu mengine ya mfuko huo ni kuagiza na kusambaza vifaa vya michezo hasa kwa watoto wadogo (grassroots) na vijana.

Mfuko huo utazinduliwa Oktoba 8 mwaka huu ambayo ni siku ya kilele cha Tanzania kutimiza miaka 50 ya uanachama wake katika Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA).

Mbali ya Tenga, wajumbe wengine wanaounda bodi ya mfuko huo ni Mwenyekiti wa zamani wa Simba, Ayoub Chamshama, Katibu Mkuu wa zamani wa TFF, Fredrick Mwakalebela, Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha, Tarimba Abbas na Mbunge wa Viti Maalum, Zarina Madabida.