Tuesday , 8th Jul , 2014

Wakati Taifa Stars inaingia kambini Tukuyu mkoani Mbeya kesho (Julai 9 mwaka huu), kocha Mart Nooij amesema kambi ya wiki mbili nchini Botswana imekisaidia kikosi chake kujiandaa kwa ajili ya mechi dhidi ya Msumbiji.

Kikosi cha timu ya Taifa ya Tanzania taifa stars kitakachowakabili Mambaz ya Msumbiji Julai 20 mwaka huu.

Kocha mkuu wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania taifa stars mdach Mart Nooij amesema ziara ya kambi ya mafunzo na michezo ya kirafiki walioifanya kwa wiki mbili nchini Botswana imempa fulsa ya kufanyia marekebisho mapungufu ya kikosi hicho kabla ya kuwavaa Mambaz ya Msumbiji julai 20 mwaka huu jijini Dar es salaam
Nooij amesema hana wasiwasi na Msumbiji kwakua anaifahamu vema timu hiyo na aina ya mchezo wao kitu ambacho kitamrahisishia kupata matokeo mazuri siku hiyo

Aidha Nooij amesema atatumia mitindo na staili tatu tofauti za uchezaji ili kuhakikisha kikosi cha stars kinaibuka akitumia staili ya kushambulia kwa kustukiza , kujilinda na kumiliki zaidi mpira

Kwa upande wake nahodha wa taifa stars beki kisiki Nadil Haroub ‘canavaro’ akiongea kwa niaba ya wachezaji wenzake amesema wao kama wachezaji wanajua umuhimu wa mechi hiyo dhidi ya Msumbiji na kwakulitambua hilo wanajipanga kucheza kufa na kupona ili kuhakikisha wanaibuka na ushindi na kujiweka katika mazingira yakucheza hatua ya makundi ya fainali za afrika AFCON michuano itakayofanyika mwakani nchini Morocco

Kwa upande mwingine timu ya taifa stars inataraji kuelekea tukuyu wilayani Lungwe jijini Mbeya tayari kwa kambi ya wiki mbili ikijiwinda na mchezo wa kwanza wa kuwania tiketi ya kufuzu mataifa ya afrika AFCON dhidi ya Msumbiji mchezo utakaopigwa julai 20 katika uwanja wa taifa jijini Dar es salaam

Ambapo Daktari wa timu hiyo Bile Haonga anatoa ufafanuzi na kueleza faida za timu hiyo kwenda kufanya mazoezi mbeya ambako kunabari kali badala ya kuweka kambi hapa jijini Dar es salaam ambako ndiko kutafanyika mchezo huo
Aidha Dr. Bile amesema kisayansi kuipeleka timu hiyo katika eneo ambalo liko ukanda wa juu litaisaidia timu hiyo kufanya vema hasa ikizingatiwa mchezo utachezewa eneo ambalo ni ukanda wa chini

Stars inataraji kuondoka na wachezaji 25 ambao ni Aggrey Morris, Aishi Manula, Amri Kiemba, Benedictor Tinoko, Deogratius Munishi, Edward Charles, Emmanuel Namwando, Erasto Nyoni, Haruni Chanongo, Himid Mao, John Bocco na Jonas Mkude.

Wengine ni Joram Mgeveke, Kelvin Friday, Kelvin Yondani, Khamis Mcha, Mrisho Ngasa, Mwagane Yeya, Nadir Haroub, Oscar Joshua, Pato Ngonyani, Ramadhan Singano, Said Juma, Said Moradi, Shabani Nditi, Shomari Kapombe, Simon Msuva,

Wakati huo huo shirikisho la soka nchini Tanzania TFF limesema tayari limeshafanya utaratibu wa kuhakikisha wachezaji wa kimataifa wa Tanzania Mbwana Samata, Thomas Ulimwengu na Mwinyi Kazimoto wanawasili nchini mapema kuikabili Msumbiji

Afisa habari wa TFF Boniface Wambura amesema kwakuzingatia umuhimu wa mchezo huo na mahitaji ya kocha tayari wameshatuma barua za kuwahitaji wachezaji hao watatu katika vilabu vyao na TFF wanamatumaini wachezaji wao kuwepo katika mchezo huo katika muda muafaka.