Saturday , 9th Jan , 2016

Simba SC itakutana na Mtibwa Sugar katika Nusu Fainali ya Kombe la Mapinduzi Jumapili, Uwanja wa Amaan, Zanzibar, wakati URA ya Uganda itamenyana na Yanga SC.

Hiyo inafuatia Simba SC kumaliza kileleni mwa Kundi A baada ya leo kuifunga JKU 1-0 katika mchezo wa mwisho wa hatua ya makundi ya michuano hiyo.

Bao pekee la mabingwa hao watetezi, limefungwa na kiungo Jonas Gerald Mkude dakika ya 64, akimalizia krosi ya beki mrundi, Emery Nimubona kutoka upande wa kulia.

Endapo mchezo huo ungemalizika kwa sare yoyote, Simba ingemaliza mechi za makundi ikiwa nafasi ya pili hivyo ingekutana na Yanga kwenye mchezo wa nusu fainali ambayo imeongoza kundi B.

Simba SC ilionesha kutafuta ushindi tangu mwanzo mwa mchezo kwani iliweza kupata nafasi nyingi lakini ilishindwa kuzitumia.

Mshambuliaji Mkenya Paul Raphael Kiongera alikaribia kufunga dakika ya 12 kama si kupiga vibaya shuti lake akiwa ndani ya 18, kufuatia krosi ya mshambuliaji Mganda, Hamisi Kizza.

Kizza naye alichelewa kuunganisha krosi ya winga mganda mwenzake, Brian Majwega dakika ya 24, wakati Kiongera alidondoka na kushindwa kuunganisha krosi Kizza dakika ya 44.

Sekunde chache kabla ya mapumziko, almanusra JKU wapate bao kama si kipa wa Simba SC, Peter Manyika kudaka shuti la mpira wa adhabu la Khamisi Makame.

Kipindi cha pili kilianza kwa timu zote kuonyesha kuwa na kika ya 60 Kiungo Said Hamisi Ndemla alipiga pembeni akiwa amebaki na kipa na Mohammed Abrahman kufuatia kazi nzuri iliyofanywa na Ibrahim Hajib.

Mbarouk Fakhi aliikosesha JKU bao la kusawazisha dakika ya 80 baada ya kupiga juu akiwa eneo la hatari kufuatia pasi nzuri ya Khamis Khamis.

Kutoka Kundi A, JKU na Jamhuri zote zimeyaaga mashindano huku Simba SC na URA zikitinga Nusu Fainali, wakati Kundi B Azam FC na Mafunzo zimetolewa, huku Yanga na Mtibwa wakisonga mbele.

Kikosi cha Simba SC kilikuwa; Peter Manyika, Emery Nimubona, Brian Majwega/Joseph Kimwaga dakika 76, Abdi Banda, Hassan Isihaka, Jonas Mkude, Awadh Juma/Mwinyi Kazimoto dk46, Said Ndemla, Paul Kiongera/Ibrahim Hajib dk46, Peter Mwalyanzi/Mohammed Fakhi dk76 na Hamisi Kizza/Danny Lyanga dk46.

JKU; Mohammed Abrahman, Ponsiana Malik Jose, Abdallah Waziri Suleiman, Khamis Abdallah Ali, Issa Haidari Dau, Khamis Said Khamis, Isamil Khamis Amour, Emmanuel Martin Joseph, Ally Vuai Hassan/Mbarouk Fakhi dk46, Khamis Mussa Makame/Feisal Abdallah dk71 na Mohammed Abdallah/Salum Salum dk71.