Thursday , 14th Apr , 2016

Rais wa chama cha soka Zanzibar (ZFA) Ravia Idarous Faina amechaguliwa tena kushika wadhifa huo baada ya kumbwaga mgombea mwenzake kocha wa zamani wa timu ya taifa ya Zanzibar Salum Bausi Nassor.

Katika uchaguzi huo Ravia ameshinda kwa kupata kura 47 huku Bausi akiwa na kura 6.

Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya ZFA Suleiman Haji Hassan “Kibabu”, alimtangaza Ravia kuwa mshindi baada ya kupata idadi ya kura hizo ambazo ni sawa na asilimia 88.68 ya kura zote 53 zilizopigwa katika mkutano huo uliofanyika katika ukumbi wa uwanja wa Gombani kisiwani Pemba

Kwa upande mwingine Mwenyekiti huyo amemtangaza aliyekuwa Makamu wa Rais wa chama hicho kisiwani Pemba Ali Mohammed Ali kutetea kiti chake kwa kumshinda Suweid Hamad Makame baada ya kupata kura 46 (86.79%) dhidi ya 7 (asilimia13.21) za mpinzani wake.

Kwa upande wa nafasi ya Makamu wa Rais wa ZFA Unguja, Katibu Mkuu wa zamani wa chama hicho Mzee Zam Ali alitangazwa kuwa mshindi baada ya kupata kura 37 sawa na asilimia 69.81 dhidi ya kura 11 sawa na asilimia 20.76 alizopata Mohammed Masoud Rashid na kura 5 alizopata Ali Nassor Salum ‘Mkweche’ambazo ni sawa na asilimia 9.43.

Viongozi hao watakaa madarakani kwa muda wa miaka miwili na nusu badala ya miaka minne kufuatia wajumbe wa mkutano huo kukubaliana kutokana na kuwa kipindi cha mwaka mmoja na nusu uliopita kutumika bila kufanyika uchaguzi ktokana kuwepo kwa kesi katika mahakama za kiraia.