Monday , 29th Dec , 2014

TIMU ya Mbeya City ya jijini Mbeya imesema bado ina nafasi nzuri ya kuhakikisha wanafanya vizuri katika mechi zilizobakia za ligi kuu Tanzania Bara.

Akizungumza na East Africa Radio, Msemaji wa Mbeya City, Dismas Ten amesema baada ya kumaliza mechi ya jana dhidi ya Ndanda na kuibuka na ushindi wa bao 1-0 ambao umewafikishia Point 8 katika mechi 8, timu imeendelea na mazoezi kwa ajili ya maandalizi ya mechi dhidi ya Yanga itakayochezwa Jumamosi Uwanja wa Sokoine mjini hapo.

Ten amesema mchezo huo utakuwa ni mgumu kwa upande wao kutokana na kila timu kuhitaji point Tatu muhimu kwa ajili ya kujiweka katika nafasi nzuri lakini anaamini kutokana na maandalizi ya timu hiyo itaweza kuibuka na ushindi.

Ten amesema hivi sasa kocha ana programu mpya ambayo anaamini itaweza kuwajenga wachezaji hao ili kuweza kuwaweka vizuri katika mechi mbalimbali zilizobakia kwa ajili ya kujihakikishia ushindi.

Kwa upande mwingine, Ten amesema suala la baadhi ya timu kulalamikia waamuzi kutoa matokeo kwa timu mojawapo zinapokuwa uwanjani siokweli kutokana na waamuzi hao kuchezesha kwa kufuata sheria ambapo amewashauri viongozi wa timu kufuata sheria pale wanapoona wanaonewa ili kuweza kuepusha vurugu zinazoweza kutokea.