Tuesday , 10th Nov , 2015

Vyombo vya habari nchini vimepongezwa kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kutoa taarifa kwa wananchi wakati wa uchaguzi mkuu uliofanyika mwishoni mwa mwezi wa 10 mwaka huu.

Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Vijana, wa Wizara ya Habari, Vijina, Utamaduni na Michezo Prof Elisante Ole Gabriel.

Pongezi hizo zimetolewa leo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Prof. Elisante Ole Gabriel wakati akiongea na viongozi wa menejimenti ya wizara na taasisi zake kwenye kikao cha kazi kilichofanyika jijini Dar es Salaam.

Prof. Gabriel amesema kipindi cha uchaguzi vyombo vya habari vilifanya kazi kubwa ya kuwahabarisha wananchi habari za uchaguzi kwa kuzingatia weledi wa taaluma yao na hivyo kuwawezesha wananchi kujua mambo mbalimbali yaliyokuwa yakiendelea hapa nchini.

Katibu mkuu huyo ambaye hicho kilikuwa ni kikao chake cha kwanza tangu ateuliwe kuwa katibu mkuu wa wizara hiyo mwishoni mwa mwezi wa kumi aliahidi kuwatumikia na kuwaheshimu wafanyakazi wa wizara yake huku akisimamia majukumu ya kazi kwa kufauata kanuni, taratibu na sheria za utumishi wa umma.

“Hiki ni kikao chetu cha kujipanga kwa ajili ya kazi, ni vyema tukajipanga huku tukijua matarajio ya Mhe. Rais kwetu ni yapi, wananchi tunaowatumikia wanategemea kupata nini kutoka kwetu na mimi kama katibu mkuu natarajia kupata nini kutoka kwenu”, Prof. Gabriel alisema.

Akimkaribisha katibu mkuu huyo kuongea na viongozi hao Kaimu Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu Titus Mkapa alisema kikao hicho ni maalum kwa ajili ya wizara kujadili utekelezaji wa mipango ya wizara kwa kasi.

Wakitoa maoni yao kwa nyakati tofauti viongozi hao waliiomba serikali iangalie upya bajeti ya wizara hiyo ambayo ni ndogo ili iweze kuongezwa na kuwawezesha kufanya kazi zao kwa ufaisi zaidi.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TasuBa) Michael Kadinde alisema chuo hicho kimekuwa kikizalisha ajira kwa wanafunzi wanaosoma hapo mara baada ya kumaliza masomo yao lakini wanafunzi wengi wanakabiliwa na changamoto ya kutokuwa  na ada.

“Kuna baadhi ya wanafunzi wanajiunga na chuo hiki wakiwa na elimu ya darasa la saba, na hivi sasa serikali itaanza kutoa elimu bure kwa wanafunzi kwa darasa la kwanza hadi kidato cha nne”.

“Ninaiomba serikali iweze kuwaangalia wanafunzi hawa wa darasa la saba ambao wanasoma chuoni kwetu ili nao waweze kupata elimu bure sawa na wanafunzi wa sekondari”, alisisitiza Kadinde.

Kikao hicho kimeitishwa kufuatia kikao cha Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli na Makatibu wakuu, manaibu makatibu wakuu na watendaji wakuu wa serikali  kilichofayika mwishoni mwa wiki ambapo alieleza matarajio yake na matarajio ya wananchi katika uongozi wake. Hivyo aliagiza kila sekta ikae na kujipanga kufanya kazi ili kukidhi matarajio ya wananchi.