Sunday , 5th Jul , 2015

Shirika la kuhudumia watoto ulimwenguni (UNICEF) kupitia Benki ya Dunia kwa kushirikiana na Serikali idara ya maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu imeanza kutekeleza mradi wa kuijengea jamiii uwezo wa kukabiliana na kupunguza athari za maafa.

Katibu Tawala wa Mkoa Severine Kahitwa (mwenye shati Jeupe) akizungumza na wadau wa maendeleo.

Katibu Tawala mkoani Kilimanjaro Severine Kahitwa ameyasema hayo wakati akifungua semina ya siku tatu ya mafunzo na nadharia na vitendo na tathimini ya haraka ya hali ya chakula na lishe kwa waratibu wa maafa na wakuu wa idara kutoka wilaya za Same,Mwanga na Hai, zilizopo mkoani hapa.

Alisema mradi huo unawalenga ni vikundi vya wanawake na vijana vinavyojihusisha na kilimo na ufugaji na shule za msingi zinazojihusisha na utunzaji wa bustani za miti kwa ajili ya utunzaji wa mazingira na kwamba mradi huo umetoa mbuzi 400 na kuku 500 wa kienyeji na mashine za kuangulia mayai (Incubators) 5.

Katika mradi huo pia mashine za kuchakatia mihogo 7,tani 100 za mbegu za mihogo,tani 88 za mbegu za viazi ,kilo 300 za mbegu za miti aina mbali mbali na tani tatu za mbegu za mtama na migomba zilizosambazwa kwa vikundi hivyo.

Alisema ili kufanikisha mradi huo vikundi hivyo vimepatiwa vitendea kazi vya kutekeleza mradi huo yakiwemo majembe ya mikono kumi ,mapanga kumi,Glovu pea kumi na mabomba tisa ya kunyunyuzia dawa mazao mashambani.

Mradi huo pia umetoa vifaaa vya kujenga uzio wa vitalu vya miti kwa shule tatu ikiwa ni pamoja na kuwawezesha waratibu wa halmashauri kuwa na vitendea kazi kama Kompyuta 4 za mpakato ,na kompyuta nne za mezani kitunza umeme nne ,simu za mkononi ,kamera za video na kamera za picha mnato.

Vifaa hivyo vimekuwa msaada mkubwa katika utendaji na kuwa na mafanikio ya mradi huu ni pamoja na mbuzi 78 zimeongezeka,kuku 354 na mayai 1,119 wakati miche 22,578 ya miti imeoteshwa katika maeneo mbali mbali yakiwemo mashule ,maeneo ya wazi ,vilele vya milima na katika maeneo ya vyanzo vya maji.

Kahitwa alisema Jumla ya ekari 12 zimelimwa mihogo, ekari kumi na tano viazi vitamu na mtama na wakulima wa mboga mboga wamepata shilingi 9,500,000 kwa kuuza nyanya,hoho,nyanya chungu,mchicha na bilinganya.

Mradi umepanga kuwawezesha jumla ya wananchi 2,050 kupata maji safi na salama ya kunywa katika kijiji cha vunta kata ya vunta wilayani Same mkoani Kilimanjaro.