Sunday , 26th Apr , 2015

Baadhi ya mashirika ya umoja wa mataifa yanayofanya kazi zake nchini Tanzania yamesema yatahakikisha yanaendelea kulinda haki za binadamu hasa katika kipindi hiki ambapo Tanzania inaelekea kufanya uchaguzi mkuu mwezi Oktoba mwaka huu.

Mwakilishi wa umoja wa mataifa anayeshughulikia sera na utetezi wa haki za binadamu Bi. Chitralekha Massey amesema hayo leo jijini Dar es salaam wakati wa mkutano wa wadau wanaojishughulisha na utetezi wa haki za binadamu kutathimini utekelezaji wa mikataba 107 ya haki za binadamu ambayo Tanzania imesaini

Kwa upande wake Mwenyekiti wa mtandao wa watetezi wa haki za binadamu Bi. Martina Kabisama pamoja na mkurugenzi wa mtadao huo Bw. Onesmo Olengurumwa wamesema kama mshirika yasiyo ya kiserikali wana wajibu wa kutathimini namna serikali inavyotekeleza mikataba ya haki za binadamu kwa lengo la kukosoa pale ambapo patakuwa hapajafanyiwa kazi.

Kauli hiyo ya mashirika ya Umoja wa Mataifa imekuja takribani siku moja baada ya wakazi wa wilaya ya Ngorongoro kaskazini mwa Tanzania kuandamana wakidai kufanyiwa unyanyasaji na maofisa kutoka idara ya Uhamiaji wakidaiwa kuwa wao eti sio raia wa Tanzania.

Wakizungumza na vyombo vya habari, wakazi hao wameshangazwa na madai kuwa wao sio Watanzania, ambapo wametoa baadhi ya vielelezo wakionyesha kuwa wao ni raia halali wa nchi hii, vielelezo hivyo ni pamoja na nyadhifa walizowahi kushika ndani ya serikali na chama tawala CCM.