Wednesday , 3rd Aug , 2016

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amemuagiza Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), kurekebisha mapungufu ya kiutendaji ili kuondokana na matumizi mabaya ya fedha.

Waziri Mbarawa ametoa agizo hilo mara baada ya kukagua shughuli za utendaji wa bandari ya Kasanga iliyopo mkoani Rukwa inayohudumia mkoa wa Kigoma, nchi ya Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) ambapo ameyataja mapungufu hayo ikiwemo malipo yasiyotumia njia za kielektroniki na miundombinu isiyo rafiki katika kukidhi ushindani wa kibiashara katika bandari hiyo.

Prof. Mbarwa ameongeza kuwa TPA imekuwa na wajibu mkubwa wa kuchangia pato la Taifa kupitia huduma za upakiaji na upakuaji wa mizigo hivyo wanapaswa kuanza kutumia mfumo wa kielekroniki katika ukusanyaji wa mapato katika bandari zote nchini ili kudhibiti upotevu wa mapato.

Waziri Mbarawa ameitaka TPA kuweka mfumo wa uendeshaji vikao kwa njia ya kieletroniki (video conference) kwa lengo la kudhibiti matumizi ya fedha nyingi zilizokuwa zikitumika katika uendeshaji wa vikao hivyo.

“Nataka TPA muanze kutumia video Conference katika vikao vyenu ili fedha zilizokuwa zikitumika zifanyie kazi nyingine za maendeleo ya Taifa”, amesema Waziri Prof. Mbarawa.

Katika hatua nyingine Profesa Mbarawa amekagua barabara ya Sumbawanga-Matai-Kasanga Port yenye urefu wa KM 112 inayojengwa kwa kiwango cha Lami na kumtaka Mkandarasi wa barabara hiyo China Railway 15 Bureau Group Corporation kukamilisha ujenzi huo ifikapo Julai mwakani.

Amesema kukamilika kwa barabara hiyo kutaunganisha mji wa Sumbawanga na Bandari ya Kasanga na hivyo kurahisisha shughuli za usafirishaji wa abiria na mizigo kutoka bandarini hapo na hivyo kuwa kichocheo cha ukuaji wa uchumi katika Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini.