Friday , 21st Nov , 2014

Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa (TALGWU) nchini, kimeitaka serikali kuhakikisha inalipa madai ya wanachama wake yanayofikia kiasi cha shilingi bilioni 18 ,yanayotokana na malimbikizo ya mishahara,uhamisho na masomo.

Wanachama wa chama cha Wafanyakazi wa Serikali za mitaa nchini Tanzania wakiwa katika maandamano ya amani.

Akizungumza jana katika mkutano uliowakutanisha viongozi mbalimbali wa TALGWU, Jijini Arusha, Mwenyekiti wa chama hicho,Seleiman Kikingo ametoa tamko hilo, huku akisisitiza kuwa madai hayo yamedumu kwa zaidi ya miaka mitano na serikali kupitia ofisi ya waziri mkuu ikiwa kimya.

Amesema pamoja na serikali kulipa kiasi cha shilingi bilioni 5,ikiwa ni sehemu ya deni hilo jitihada zaidi zinahitajika kuhakikisha kuwa madai yao yanakamilika kabla ya uchaguzi mkuu mwakani kufika,hatua ambayo itawawezesha kujikimu na ukata unaowakabili.

Katika hatua nyingine mwenyekiti huyo, amesisitiza kwa kuzitaka halimashauri za miji na majiji hapa nchini kuunda mabaraza ya wafanyakazi kwani katika halmashauri 167 za hapa nchini mabaraza yaliyoundwa yapo 154 na kati ya hayo mabaraza 77 ndiyo yapo hai ,huku mabaraza 73 hayapo hai.