Wednesday , 30th Nov , 2016

Serikali imesema uamuzi wa kuhamisha fedha zake kiasi cha sh. billioni 515 kutoka mabenki ya biashara na kupeleka Benki Kuu ya Tanzania (BOT) hakihusiani na mzunguko mdogo wa fedha uliopo sasa bali hali hiyo inatokana na mikopo mibovu ya mabenki hayo

Msajili wa Hazina, Lawrence Mafuru

Akiongea na waandishi wa habari Msajili wa Hazina, Bwana Lawrence Mafuru amesema mabenki yalikopesha kiasi cha shilingi trilioni 16.7, kati ya hizo zaidi ya shilingi trilioni 1.43 hazijarudishwa.

Ameongeza kuwa Benki Kuu inajiendesha kulingana na mifumo ya kibenki hivyo taasisi hizo zina nafasi ya kukopa kutoka Benki Kuu.

Msajili huyo wa hazina amesema, si sahihi kwa taasisi za serikali kuhifadhi fedha katika akaunti za muda maalum (Fixed Deposit) wakati serikali inahitaji fedha kwa ajili ya mahitaji muhimu, na kuzitaka za umma kutoomba fedha kabla ya kukamilisha taratibu za manunuzi.

Bwana Mafuru amesema, kwa sasa serikali imewekeza fedha nyingi katika miradi mikubwa ya maendeleo ambayo manufaa yake hayataonekana kwa sasa hadi pale nchi itakapo jitosheleza kiuzalishaji na kimahitaji.