Wednesday , 30th Nov , 2016

Kamati ya Umoja wa Mataifa ya kutokomeza ubaguzi wa rangi imeitaka serikali ya Burundi kuchukua hatua ili kuwalinda raia ikiwemo kuruhusu mara moja kikosi cha polisi wa Umoja wa Mataifa kufuatilia usalama na hali ya haki za binadamu nchini humo

Rais wa Burundi Pierre Nkurunzinza

 

Kamati hiyo katika uamuzi iliyotoa chini ya onyo lake la kwanza na la utaratibu wa haraka wa kuchukua hatua imesema Kutokana na ukweli kwamba wanamgambo wenye silaha wanatoa vitisho vya wazi kwa watu, inaonesha, kutokuwa na nia au kukosa uwezo wa serikali kuwalinda raia.

Pia imeonesha wasiwasi wake wa kina kuhusu dodoso iliyotolewa Novemba 8 kwa wafanyakazi wa umma ikiwataka watumishi hao kuelezea hali ya ukabila wao.

Kwa mujibu wa Anastasia Crickley mwenyekiti wa kamati hiyo, kutokana na historia ya Burundi ya mgogoro wa kikabila dodoso hizo zinaweza kuzusha hofu na kutoaminiana miongoni mwa watu na inaweza kuwa hatari kubwa endapo hazitoshughulikiwa ipasavyo.

Ameongeza kuwa hali ya Burundi bado ni tete na serikali ni lazima ijiepushe na hatua zozote zitakazozorotesha zaidi hali ya kuleta mvutano wa kikabila.