Monday , 22nd Oct , 2018

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako amewaonya wahasibu wanaohudumu kwenye wizara yake ambao wamekuwa wakitumia taaluma zao vibaya kwa ajili ya kuihujumu serikali kwa kufanya malipo kinyume na taratibu zilizowekwa na kuiingizia serikali hasara.

Waziri wa Elimu Prof. Joyce Ndalichako

Waziri Prof. Ndalichako ametoa kauli hiyo jijini Dar es salaam wakati akifungua mafunzo maalum kwa wahasibu wa serikali walio kwenye wizara hiyo yenye lengo la kuwejengea uzoefu wa utendaji kazi yaliyofanyika katika Chuo cha Kodi jijini Dar es salaam.

"Kuna baadhi ya wahasibu wanatumia vibaya nafasi zao kwa kughushi nyaraka hasa kwenye masuala ya mafunzo, mara nyingi wanachezea ripoti za washiriki sasa hivi kuna ukaguzi maalum unafanyika niwaambie wahasibu ambao si waaminifu wataelekezwa kifungoni", amesema Ndalichako.

Aidha Ndalichako amesema “wahasibu wengi walidhani labda serikali imelala usingizi niwaambie tu muwe makini na kazi tumeaminiwa na serikali, naamini mwezi wa 11 tutapata ripoti na tutaweka bayana wahasibu ambao si waaminifu,."

Lakini pia kuna baadhi ya malipo ambayo yamekuwa yakifanyika kwa mkono na ukichunguza sana utagundua ni majina ya wahasibu na utakuta jina la mtu mmoja linajirudia zaidi ya mara tatu." Ameongeza Ndalichako