Thursday , 18th Feb , 2016

Hali ya hatari imeibuka katika kijiji cha Kutishi mpakani mwa wilaya za Kondoa na Simanjiro baada ya watu wa jamii ya kifugaji kutoka makabila ya maasai na watatoga kutaka kupambana kwa madai ya kuibiana ng’ombe.

Mbunge wa Simanjiiro James Ole Milya akizungumza na wananchi wake

Wanakijiji hao wengi wao wakiwa na silaha za jadi na za moto walianza kurushiana maneno hali iliyo lilazimu jeshi la polisi kuingilia kati kutuliza ghasia hizo huku ikidaiwa watu watatu yaani maasai wawili na mtatoga wamefariki dunia katika ugomvi huo.

Wanakijiji hao walikuwa wamesimama tofauti ya mita miambili na jeshi la polisi likiwa katikati kuzuia wasikaribiane huku kila maasai akidai hawataondoka bila kupatiwa ng’ombe wao na watatoga wakidai ndugu yao anadaiwa kuuawa.

Katika tukio hilo viongozi wa mila kutoka jamii hizo walitumia nguvu kubwa kuwatuliza vijana waliokuwa na jazba ambao walitaka kuvamiana wakiwa katika eneo la mbuga Tambalale katika pori la akiba la Mkungunero.

Mbunge wa Simanjiiro James Ole Milya ameitaka serikali kutopuuzia hali hiyo kwakuwa imeonesha kila dalili za uvunjifu wa amani na hali inaweza kuwa mbaya zaidi kwani kila dakika zinavyo kwenda ndiyo watu wanavyobadilika.