Sunday , 8th May , 2016

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi, Technolojia na Ufundi Injinia Stella Manyanya amesema kwamba wananchi wote watakao waozesha wanafunzi serikali ya awamu ya tano itawachukulia hatua kali za kisheria mara moja.

Injinia Manyanya ameyasema hayo alipokuwa akizungumza na walimu na wanafunzi na baadhi ya wazazi katika shule ya Sekondari Mnarani Jijini Mwanza ambayo shule hiyo ilimtoa Balozi wa watoto Getrude Clement ambaye aliiwakilisha nchi na kuhutubia katika mkutano wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki za watoto jijini New York Marekani mbele ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki- Moon.

''Kuna tabia za ajabu za wazazi kujifanya wamemuhamisha mtoto kwenda shule nyingine kumbe wamemuozesha , sasa hivi ole wake mzazi atakayethubutu kumuozesha binti anayesoma serikali itawachukulia wazazi hatua kali za kisheria''- Amesema Manyanya.

Aidha Naibu Waziri huyo amempongeza mwanafunzi huyo Getrude Clement , walimu na wanafunzi wa shule ya Sekondari Mnarani kwa kuifanya ijulikane katika ramani ya dunia.