Thursday , 26th May , 2016

Mshauri maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Burundi Jamal Benomar anasafiri leo kwenda mji mkuu Bujumbura kufuatia mazungumzo yaliyofanyika awali wiki hii mjini Arusha Tanzania kuhusu mchakato wa kisiasa nchini Burundi.

Mshauri Maalum wa UM Jamal Benomar na Rais mstaafu na Msimamizi wa mazungumzo ya Burundi Benjamin Mkapa.

Msemaji wa Umoja wa Mataifa Farhan Haq amesema hayo leo akizungumza na waandishi wa habari mjini New York Marekani, na kuongeza kwamba Bw. Benomar amejadiliana na wadau mbalimbali kwenye mazungumzo hayo na kusisitiza umuhimu wa mchakato jumuishi ili kupata mustakhabali wa amani kwa Burundi.

Kupitia akaunti yake ya Twitter, Bw. Benomar amesema ,anatumai mazungumzo ya Arusha yatakuwa hatua ya kwanza katika kufanikisha huo mchakato.

Ameongeza kuwa hiyo ni changamoto kubwa na yeye pamoja na timu yake wako tayari kusaidia juhudi za msimamizi wa mazungumzo Bw. Benjamin Mkapa.

Pia amepongeza Bw. Mkapa kwa jitihada zake akiunga mkono uamuzi wake wa kukutana na wadau wa Burundi waliokataa kuhudhuria mazungumzo ya Arusha.