Wednesday , 11th Jun , 2014

Hatimaye mgomo wa daladala uliodumu kwa siku 2 mjini Mbeya wamalizika leo baada ya mazungumzo kufanyika kati ya madereva na halmashauri ya jiji.

Moja ya dalada iliyoanza kufanya kazi leo jijini Mbeya

Madereva wa daladala ambao wamekuwa kwenye mgomo kwa siku mbili  jijini mbeya, hatimaye wameamua kusitisha mgomo wao na kurejea barabarani kutoa huduma ya usafiri baada ya serikali kuahidi kushughulikia malalamiko yao ifikapo June 12, mwaka huu.

Mabasi hayo leo yameonekana barabarani yakitoa huduma ya usafiri kwa wananchi, ambapo viongozi wa madereva hao wamesema kuwa uamuzi wao wa kusitisha mgomo unatokana na ahadi ambayo wamepewa na serikali ya kushughulikia madai yao ifikapo kesho.

Kaimu mkurugenzi wa jiji la mbeya, Dkt Samwel Lazaro amesema kuwa wamekubalian kufanya upya tathimini ya njia mpya kwa lengo la kujiridhisha kama madai ya madereva hao ni ya msingi  ili waweze kuchukua hatua stahiki.

Madereva hao wa dalada wanapinga mabadiliko ya njia mpya ambazo wamepangiwa na mamlaka ya udhibiti wa usafiri wa majini na nchi kavu (SUMATRA) kwa madai kuwa njia hizo ni ndefu ikilinganishwa na nauli inayotozwa, hali ambayo inawafanya waendeshe biashara hiyo kwa hasara.