Wednesday , 8th Oct , 2014

Tanzania ina zaidi ya watu 450,000 wenye matatizo ya afya ya akili ambao wengi wao ni vijana wenye umri wa kuanzia miaka 15 na kuendelea tatizo lililotajwa kusababishwa na matumizi ya madawa ya kulevya ikiwemo uvutaji wa bangi.

Mganga Mkuu wa Serikali nchini Tanzania, Dkt Donan Mmbando.

Mganga mkuu wa serikali Dkt. Donald Mbando ametoa takwimu hizo leo wakati akiongea na waandishi wa habari kueleke maadhimisho ya siku ya Afya ya akili duniani ambayo kitaifa yataadhimishwa tarehe 10 mwezi huu katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es salaam.

Dkt. Mbando amesema ugonjwa wa afya ya akili pia umekuwa ukiwakumba wazee ambapo umekuwa ukiathiri uwezo wa mtu kufikiri, kuhisi, kutambua na kutenda na hivyo kuwa na mwenendo au tabia tofauti usioendana na jamii na kushauri kufikishwa mara moja katika vituo vya afya au hospitali kwa mtu mwenye dalili kama hizo.

Aidha imeelezwa kuwa Tanzania kwa sasa inagundua wagonjwa wapya 5000 wa ugonjwa wa Saratani kila mwaka ikiwa ni asilimia 10 pekee ya wale ambao wanaweza kufika hospitalini, huku ikielezwa kuwa silimia 70 ya wagonjwa wa saratani duniani wanakufa kila mwaka.

Akizungumza na EATV, daktari bingwa upande wa udhibiti wa saratani kutoka Taasisi ya Saratani ya Ocean Road ya jijini Dar es salaam Dkt Chrisphin Kahesa, amesema kuwa ugonjwa huo unasababishwa na matumizi mabaya ya chakula pamoja na matumizi ya kemikali kupitia vipodozi na matumizi ya tumbaku.

Aidha Dkt Kahesa ameitaka serikali na taasisi binafsi kuweka sera itakayowezesha Hospitali mbali mbali kubadilisha mtazamo wa kutibu peke yake bali kuzuia kuenea kwa ugonjwa huo ikiwemo kupunguza gharama za matibabu,jitihada hizo zitasaidia katika kuokoa maisha kwa wagonjwa wa saratani.