Jumanne , 22nd Nov , 2016

Kiungo wa Leicester City, Riyad Mahrez amesema timu hiyo haina shinikizo lolote na wapo tayari kucheza mchezo wao wa kutafuta kuingia 16 Bora ya Ligi ya Mabingwa Barani Ulaya, usiku wa leo.

Riyad Mahrez

Mabingwa hao wa Ligi Kuu ya Soka nchini Uingereza, wanashuka kwenye uwanja wao King Power kuikaribisha Club Brugge, huku ikihitaji pointi moja tu, kufuzu hatua ya mtoano, na Mahrez anaamini hilo linawezekana kwa kuwa wanauchukulia mchezo huo kama michezo mingine.

Leicester inaongoza kundi G ikiwa na pointi 10, baada ya michezo 4, ikifuatiwa na FC Porto iliyo nafasi ya pili, kwa pointi 7, na FC Koebenhavn yenye pointi 5 iliyo nafasi ya tatu, wakati Club Brugge ikiburuza mkia bila ya pointi.

Michezo mingine ya hii leo, katika Kundi H Dinamo Zagreb , itakuwa wenyeji wa Lyon , wakati Sevilla, ikiikaribisha Juventus.

Kundi F, mitanange ni pale Borussia Dortmund ikiwa nyumbani inakuwa mwenyeji wa Legia Warsaw, ilhali Sporting CP wakiipa mwaliko Real Madrid.

Kundi E, CSKA Moscow wapo nyumbani dhidi ya Bayer Leverkusen, wakati Monaco wanaipa mwaliko Tottenham Hotspur.