Jumanne , 20th Oct , 2015

Msanii Baraka De Prince ambaye anafanya vizuri na wimbo wake wa nivumilie aliomshirikisha mwanada

Msanii Baraka De Prince ambaye anafanya vizuri na wimbo wake wa nivumilie aliomshirikisha mwanadada Ruby, ameamua kurudisha fadhila kwa jamii anayotoka baada ya kupata mafanikio kupitia kipaji chake cha kuimba muziki.

Baraka ameiambia Planet Bongo ya East Africa Radio, ana mpango wa kujenga maktaba katika shule aliyosoma pamoja na vitu vingine, ukiwa kama mchango wake kwa jamii hiyo.

"Unajua mi sio mtu ambaye nafanyaga vitu but sio mtu ambaye naongea na kuzungumza sana labda kama nimefanya nini, kwa hiyo na shule ambayo mi nimesomea inaitwa Pamba primary school kuna kitu ambacho nataka nifanye, nataka nikatengeneze maabara ya vitabu kama Mungu akisaidia", alisema Baraka.

Baraka de Prince amesema amefikia kufanya hivyo kwa sababu anaipa nafasi kubwa elimu katika maisha yetu, na hususan kwa vizazi vijavyo.

"Elimu pia naipa nafasi kubwa katika maisha yangu, hususan kwa hawa watoto wetu ambao wanakuja wadogo zetu, wanatakiwa wapate elimu kwa sababu ukiwa na elimu bila hata kuajiriwa unakuwa na knowledge ya kujua hata ufanye nini na mipaka ya matumizi yako, na ufanye nini ili uweze kufanikiwa",alisema Baraka.

Licha ya kujenga maktaba shuleni hapo, Baraka anatarajia kugawa vitabu, madaftari na vifaa vingine kwa wanafunzi wanaosoma shuleni hapo.