Jumatano , 27th Mar , 2024

Waziri wa Habari Vijana utamaduni na Michezo Zanzibar Mheshimiwa Tabia Maulid Mwita, ametangaza kuwa Zanzibar imetangazwa kuwa mwenyeji wa mashindano ya Senior Challenge Cup CECAFA 2024.

Mhe. Tabia ameeleza hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi yake iliyopo Migombani Zanzibar.

Katika mkutano huo, Mhe. Waziri Ametangaza kuwa Zanzibar imebahatika kuwa mwenyeji wa Mashindano ya Challenge Senior Cup mwaka huu ambapo mashindano hayo yanatarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwezi wa Juni, 2024 katika Viwanja vya New Amani Complex.

Aidha Amempongeza na kumshukuru kwa dhati Mhe Dkt. Hussein Ali Mwinyi Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa baraza la mapinduzi kwa Maamuzi yake ya kijasiri yaliyolenga kuboresha maendeleo katika sekta ya michezo ambayo yamechochea Zanzibar kuwa wenyeji wa Michuano hayo.

Pia amesisitiza umuhimu wa maandalizi bora kwa timu za Taifa za ndani na nje ya nchi zitakazoshiriki.

Aidha, ameonyesha azma ya kuitetea tasnia ya michezo kwa kuirejesha kamati ya Saidia Zanzibar Ishinde (SAZI) ili kusaidia katika maandalizii hayo ambapo ameteua wajumbe kutoka maeneo mbalimbali.

Wajumbe walio teuliwa na Mhe. Waziri Tabia ni pamoja na, Mheshimiwa Ayoub Mohammed Mahmoud (Mwenyekiti), Ndugu Said Kassim Marine (Katibu), Mheshimiwa Nassor Ali Salim Jazira, Mheshimiwa Ussi Salum Pondeza.

Wengine ni, Mheshimiwa Fatma Ramadhan Mandoba, Ndugu Arafat Ally Haji, Ndugu Mwalimu Ali Mwalimu, Ndugu Naima Said Shaame, Ndugu Ramadhan A. Bukini, Mheshimiwa Abulghafar Idrissa Juma

Mhe. Waziri Mwita ameonyesha imani yake kwa kamati hii na ana matarajio makubwa kwamba watafanya kazi kwa bidii ili kufanikisha mashindano haya makubwa.